Niyonzima, Okwi wawapa raha mashabiki, Simba ikiisogelea Yanga kileleni

Muktasari:

  • Ushindi huo Simba imefikisha alama 63 ikijiimarisha nafasi ya tatu nyuma ya Azam FC huku  Yanga yenye alama 74 ikiwa kinara kileleni

Mwanza. Timu ya Simba imeibuka na ushindi leo Jumanne dhidi ya Alliance FC baada ya kuifunga bao 2-0 kwenye Uwanja wa Kirumba jijini Mwanza.

Bao la dakika ya 27 lililofungwa na kiungo mshambuliaji Haruna Niyonzima liliipeleka Simba mapumziko wakiwa wanaongoza bao 1-0 .

Niyonzima alifunga bao hilo dakika ya 27 akipokea krosi ya Mzamiru Yassin na kupiga shuti lililomshinda kipa John Mwanda na kujaa wavuni.

Baada ya bao hilo Alliance walifanya mabadiliko na kumtoa Richard John na kumwingiza Husein Javu ambaye aliongeza nguvu kwenye safu ya ushambuliaji.

Uimara wa kipa Aishi Manula kuokoa mashambulizi kuliwanyima bao la kusawazisha Alliance.

Kipindi cha pili timu hizo zilishambuliana kwa zamu, huku Simba ikifanya mashambulizi mengi langoni kwa Alliance.

Dakika 75 Emmanuel Okwi aliandika bao la pili akiwapangua mabeki wa Alliance FC.

 Ushindi huo Simba imefikisha alama 63 huku ikiendelea kujiimarisha nafasi ya tatu ikiwa nyuma ya Yanga na Azam.