Mapunda awashusha presha Majimaji

Muktasari:

  • Mchezaji huyo ameweka bayana kwamba masuala ya usajili wake atayaweka wazi mwisho wa msimu huu

Winga wa Majimaji, Peter Mapunda amesema kwa sasa akili yake ni kusaidia timu hiyo mambo ya usajili baadaye.

Mapunda alikuwa akihusishwa na kutaka kuachana na klabu hiyo baada ya kupata ofa kutoka katika klabu mbili za Ligi Kuu Bara.

“Nimeamua kwanza kuachana nao kwa sababu nimeona nielekeze akili yangu katika timu yangu, nataka ligi ikimalizika ndio niwasikilize tena wanasemaje, nimehofia kuchanganya mambo mengi naweza nikashusha kiwango changu, bora nimalize ligi tu,” alisema.

Akizungumzia ofa ya Yanga, alisema ni suala la kusubiri muda husika ufike ndio afanye uamuzi sahihi ya wapi asaini, lakini siyo hivi sasa.

“Akili inabidi itulie katika kufanya uamuzi, sio hao tu bali timu zimezidi kuongezeka mpaka hivi sasa, zipo za Ligi Kuu na zilizopanda pia, acha kwanza nitulie naamini nitapata timu ambayo nastahili kucheza kwa utulivu,” alisema.