Nyota wa Kagera Sugar ajiweka sokoni

Muktasari:

  • Nipo sokoni sina mkataba na wala sijapata ofa na timu yoyote hadi muda huu

Dar es Salaam. Mshambuliaji wa Kagera Sugar, Japhet Makalai amejiweka sokoni baada ya kukiri kumaliza mkataba wake na timu hiyo.

Makalai aliyefunga bao la pili katika ushindi mabao 2-1 wa mchezo wao wa mtoano 'Play Off' dhidi ya Geita Gold.

Makalai alisema anamshukuru Mungu amemaliza ligi salama ingawa hakuwa na msimu mzuri ndani ya timu hiyo kutokana na kukosa namba kikosi cha kwanza.

"Sijacheza michezo mingi ya ligi siwezi kuzungumzia ugumu wake na sababu zilizotufanya tuyumbe na kujikuta tunacheza mtoano kubwa tunashukuru tumebakisha timu Ligi Kuu."

"Nimemaliza vizuri ligi na timu yangu baada ya kuibakisha kwa kufunga bao la ushindi, lakini baada ya ushindi huo nadhani ndio ulikuwa mchezo wangu wa mwisho kwani nimemaliza mkataba na timu hiyo."

"Nipo sokoni sina mkataba na wala sijapata ofa na timu yoyote hadi muda huu kwani ndio kwanza nimemaliza ligi hivyo nahitaji kutuliza akili ili kupata timu sahihi," alisema Makalai.