VIDEO: Salamba kuomba kiatu ni gumzo kila kona mitandaoni

Muktasari:

Mchezo uliowakutanisha Mabingwa wa Tanzania Simba Sc na Sevilla ya Hispania umeacha Gumzo mitandaoni baada ya kitendo cha Mshambuliaji wa Simba Adam Salamba kuonekana akiomba Kiatu cha Star wa Sevilla Ever Banega.

Dar es Salaam. Kitendo cha mshambuliaji wa Simba, Adam Salamba kuomba kiatu cha nyota wa Sevilla ya Hispania, Ever Banega kimezua gumzo kubwa katika mitandao ya kijamii nchini.

Baada ya mechi kumalizika na Simba kuchapwa mabao 5-4, Salamba alionekana katika picha ya video iliyosambaa mitandano akijaribu kumuomba nyota huyo jezi na viatu.

Kitendo hicho kimezua mjadala kutokana na utani wa jadi baina ya mashabiki wa Simba na Yanga nchini.

Mashabiki wa Yanga wakikosoa kitendo hicho wengine wakiita ni kujidhalilsha huku mashabiki wengine wakipongeza kitendo hicho wakiita ni ushujaa wa kutaka kutunza kumbukumbu muhimu katika soka kutokana na ukubwa wa jina la star huyo Ever Banega.

Msemaji wa Timu ya Simba Haji manara katika mtandao wake wa Instagram amewajibu mashabiki wanaoonekana kukosoa kitendo cha Adam Salamba. Katika mtandao huo Manara ameandika

“Wapo wakosoaji wetu wanasema kuomba ukumbusho wa viatu ni ushamba!!
Hawana wajualo ktk football na ugeni tulionao ktk mchezo huu murua zaidi duniani!! Hebu kioneni hcho kitendo hapo,Sasa kwa level waliyonayo Sevilla ,Wachezaji wetu kutaka ukumbusho wa viatu lipi la ajabu?
Hao wanaosema hvyo ukiwauliza makwao wana ukumbusho gani muhimu watakwambia nna picha nimepiga na Wema Sepetu au Shaffi Dauda!!
Demmm” ameandika manara huku akiambatanisha na Video inayowaonyesha wachezaji wa Raja Casablanca wakingangania viatu vya Nyota wa Brazil Ronaldinho

Pamoja na Msemaji huyo wa soka Wadau wengine waliotoa maoni yao ni pamoja na Mwandishi wa Michezo Tanzania, Edo Kumwembe ambaye katika mtandao wake ameandika

Ever Banega...naliona jina hapo katika kiatu.. Kiungo wa National team Argentina.. Salamba hata Afcon haendi.. Hamuoni gap hapo? Hakuna aibu kuomba kiatu.. Wazungu wanaita souvenir..kumbukumbu ya maisha yako..tujikumbushe kwamba hata Samatta anaweza kumuomba viatu Messi.. Sio kwa sababu ya umaskini.. Sababu ya souvenir..lakini hatulioni pia gap la Sevilla na Simba? Kwamba mchezaji wa Simba ni sawa tu na wa Sevilla? Ujinga..ndo Maana hatujifunzi. Wawa katoka taifa kubwa la soka lakini kumbe aliacha simu katika benchi..akakimbilia akapiga selfie.. Wale ni Sevilla jamani..anyway nawapenda Yanga jinsi wanavyoihenyesha Simba kwa utani..wanajua jinsi ya kusahau matatizo yao na kuwachapa Simba na issue Kama hizi.. Bodaboda.. Kiatu.. Otherwise hakuna cha ajabu alichofanya Salamba..yule ni EVER BANEGA ambaye ana utajiri wa dola milioni 19 kwa mujibu wa Forbes...yeye ni Adam Salamba..anamiliki crown tu.. NIMEFUNGA KESI, ameandika Edo kumwembe Huku akiambatanisha na Picha ya kiatu cha mshambuliaji huyo wa Sevilla Ever Banega

Mtangazaji na Mchambuzi wa Soka Shaff Dauda katoka Ukurasa wake naye hakuwa nyuma kwa kuandika “Kwani kuomba viatu na jersey kipi bora? Vyote si ukumbusho au?”ikiwa ni mfumo wa swali akiwaacha mashabiki kuchangia mjadala huo ambao wameendelea kutofautiana kutokana na tukio hilo.

Katika mchezo huo pia Beki wa Pembeni wa Simba Mohammed Hussein ameonekana akiwa na T-shet ya Ever Banega ambapo katika mtandao wake wa kijamii ameandika kuwa “Ili Uwe Mkubwa Lazima Ukutane na Watu Wakubwa Alhamdullilah”

Simba ambao ni Mabingwa wa Tanzania jana walijipima nguvu na Sevilla Katika mchezo wa kirafiki ulioandaliwa na Kampuni ya Michezo ya kubahatisha na wadhamini wa timu hiyo Spotipesa .