Samatta aisaka rekodi mpya Ligi ya Mabingwa leo

Muktasari:

Msimu huu wa 2019/20, Samatta ameifungia KRC Genk mabao matano kwenye Ligi ya Ubelgiji ambayo ni maarufu kama Jupiler Pro.

Dar es Salaam. Nahodha wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, Mbwana Samatta anatarajia kuweka rekodi mpya ya kuwa Mtanzania wa kwanza leo kucheza Ligi ya Mabingwa wakati Genk itakapokuwa ugenini kuivaa Red Bull Salzburg kwenye uwanja wa  Wals-Siezenheim, Austria.

Samatta kinara wa mabao KRC Genk aliikosa mechi ya ligi Ijumaa kutokana na kuwa majeruhi, lakini amejumlisha katika kikosi cha mabingwa hao wa Ubelgiji kilichosafiriki kwenye Austria baada ya kufuzu vipimo vya afya.

Samatta alifanyiwa vipimo vya mwisho jana kabla ya kuanza safari ya kuelekea Austria, kufuatia majeraha ya goti aliyoyapata akiichezea Taifa Stars katika mchezo wa kusaka kufuzu Kombe la Dunia dhidi ya Burundi.

Awamu hiyo ilikuwa ni ya pili kwa Samatta kufanyiwa vipimo ya kwanza ilibaini kuwa hakupata majeraha makubwa na badala yake akapewa muda wa kupumzika, kilichofuata ni kujilidhisha na urejeo wake kabla ya kujumuishwa kwenye msafara.

Wakiwa na ndege mbili ambazo ni JNL972 na TB 9200, walisafiri jana mchana pamoja na kikosi chao B kutoka kwenye uwanja wa ndege wa Maastricht Aachen, Ubelgiji   hadi Salzburg nchini Austria.

Samatta akiwa na wenzake walifanya mazoezi ya mwisho usiku wa jana kwenye uwanja wa Wals-Siezenheim au Red Bull Arena ambao utatumika kwenye mchezo wa leo.

KRC Genk ipo Kundi E baada ya kucheza na Red Bull Salzburg, watarudi nyumbani kuikaribisha  Napoli  ya Italia, Oktoba 2 kabla ya  kukumbana na majogoo wa jiji Liverpool, Oktoba 23.