Samatta atinga fainali, Aston Villa yaichapa Leicester City

Muktasari:

Ushindi huo unaifanya Villa pamoja na Samatta sasa kusubiri mshindi wa mechi ya nusu fainali ya pili itakayochezwa leo Januari, 29 kati ya Manchester City dhidi Manchester United

London, England. Mshambuliaji Mbwana Samatta amekuwa mtanzania wa kwanza kucheza fainali ya Carabao kwenye Uwanja wa Wembley baada ya Aston Villa kuichapa Leicester City kwa mabao 2-1 na kusonga mbele kwa ushindi wa jumla 3-2.

Ushindi huo unaifanya Villa pamoja na Samatta sasa kusubiri mshindi wa mechi ya nusu fainali ya pili itakayochezwa leo Januari, 29 kati ya Manchester City dhidi Manchester United.

Katika mchezo huo Samatta akicheza mechi yake ya kwanza alifunga bao lakini mwamuzi alikataa akidai ameotea kabla ya kutolewa dakika ya 67 ya mchezo.

Wenyeji Aston Villa walikuwa wa kwanza kupata bao lililofungwa na Targett dakika 22, Trezeguet alifunga bao la pili dakika 90+3, huku bao la kufutia machozi la Leicester City likifungwa na Iheanacho dakika ya 72.

Katika mchezo huo macho ya watanzania wengi yalikuwa kwa Samatta ambaye alikuwa akicheza mechi yake ya kwanza tangu amejiunga na Villa akitokea Genk ya Ubelgiji.

Samatta alijitahidi kuonyesha uwezo wake, lakini alikosa nafasi mbili za wazi za kufunga katika mchezo huo uliokuwa na ushindani mkali vipindi vyote viwili.