Simba yadhihirisha ubora ikitinga robo fainali Ligi ya Mabingwa Afrika

Muktasari:

Baada ya AS Vita kupata bao la kuongoza, utulivu kwenye kikosi cha Simba ulipotea kiasi cha kuanza kuonekana tatizo kwenye eneo lao la kiungo mkabaji ambalo alikuwa akicheza James Kotei na Mzamiru Yassin.

Timu za Simba imeibuka na ushindi wa mabao 2- 1 dhidi ya AS Vita kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam,  ikiungana na Al Ahly  hatua ya robo fainali Ligi ya Mabingwa Afrika.

Mabao ya Simba yaliwekwa wavuni na Mohamed Hussen dakika ya 36 pamoja na bao la ushindi la Cleotus Chama dakika ya 89.

Bao walilotanguliwa Simba mwanzoni mwa kipindi hicho cha kwanza lilitokana na uzembe kwa kushindwa kuondoa mpira uliokuwa ukizagaa kwenye eneo lao la hatari.

Baada ya AS Vita kupata bao la kuongoza, utulivu kwenye kikosi cha Simba ulipotea kiasi cha kuanza kuonekana tatizo kwenye eneo lao la kiungo mkabaji ambalo alikuwa akicheza James Kotei na Mzamiru Yassin.

Kupwaya kwa eneo hilo kuliwapa nguvu AS Vita ambao walikuwa wakiishambulia Simba kwa mshambulizi mfululizo kupitia kwa wadhambuliaji wao, Tuisila Kisinda, Jean Makusu na Kazadi. Simba walizinduka dakika ya 36 baada ya kusawazisha bao kupitia kwa Tshabalala ambaye alimalizia mpira ambao mabeki wa AS Vital walijaribu kuukoa lakini jitihada zao hazikusaidia.

Mara baada ya kusawazisha bao hilo, Simba walizinduka na AS Vita wakaanza kucheza kwa kujilinda zaidi ndani ya dakika 10 za mwishoni mwa kipindi hicho cha kwanza.