Sven avunja mfupa uliomshinda Aussems Kombe la FA

Muktasari:

Kwa matokeo hayo, Simba itaungana na timu nyingine katika hatua ya Robo Fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho.
Saddam Sadick

Mwanza. Kocha wa Simba, Sven Vanderbroek amevunja mfupa uliomshinda mtangulizi wake, Patrick Aussems kufuatia ushindi wa penalti 3-2 baada ya dakika 90 kumalizika kwa sare ya bao 1-1.
Katika mchezo huo uliopigwa Uwanja wa CCM Kambarage mjini Shinyanga, licha ya ushindani kwa timu zote, lakini Wekundu hao waliweza kufuzu hatua ya Robo Fainali ya Kombe la Shirikisho.
Simba ilishuka uwanjani ikikumbuka kutolewa mapema msimu uliopita dhidi ya Mashujaa FC katika hatua ya 32 chini ya aliyekuwa Kocha, Atuga Manyundo ambaye leo Jumanne akiiongoza Stand United amekubali 'muziki' wa Mbelgiji huyo.
Licha ya ushindi huo, lakini Simba haikuonyesha ushindani mkali kama mechi zilizopita na kusababisha mpambano huo kuamuliwa kwa penalti.
Hassan Dilunga ndiye alitangulia kuipeleka mbele timu yake kwa kwa penalti baada ya beki wa Stand United, Antidius Ishengoma kuunawa mpira eneo la hatari.
Hata hivyo, 'Chama la Wana', halikukata tamaa na kupambana hadi kuweza kusawazisha bao hilo kupitia kwa Miraji Salehe na kufanya mchezo huo kumalizika dakika 90 kwa sare ya bao 1-1.
Kama haitoshi, Dilunga ndiye aliweza kuipeleka timu yake hatua inayofuata baada ya mkwaju wake wa penalti kukamilisha idadi ya mikwaju mitatu sambamba na ya Deo Kanda na Clatous Chama, huku Meddie Kagere na Ibrahim Ajibu wakikosa.