Tamasha la filamu la Cannes kujaa nyota wa muziki

Muktasari:

Tamasha hilo kubwa kuliko yote ulimwenguni litaanza kesho nchini Ufaransa na filamu nyingi zitakazoonyesha zimeshirikisha wanamuziki.

Bono, Elton John, Iggy Pop na Tom Waits watapita katika zulia jekundu wakati tamasha kubwa la filamu la Cannes litakaposhirikisha wanamuziki nyota wa rock ulimwenguni.
Orodha ya nyota hao pia inammjumuisha nyota wa kike wa muziki, Rihanna na wanamuziki wawili waliosalia wa kundi la Led Zeppelin ambao watakuwepo katika tamasha hilo linaloanza kesho Jumanne.
Hata filamu ya kwanza kuonyeshwa katika tamasha hilo "The Dead Don't Die (Wafu Hawafi)" imeshirikisha wanamuziki kadhaa nyota ambao kwa sasa wanafanya vizuri.
Pamoja na Waits na Iggy Pop -- walioigiza filamu hiyo -- pia wamo waimbaji nyota kama Selena Gomez na rapa RZA.
Muongozaji wa filamu hiyo, Jim Jarmusch pia hutumia muda wake wa ziada kutunga nyimbo wakati waigizaji wengine nyota, Bill Murray na Adam Driver pia ni wanamuziki.
Elton John ameahidi kupiga piano yake kubwa wakati wa uzinduzi wa filamu ya "Rocketman".
Huku filamu ya "Bohemian Rhapsody" ikiingiza zaidi ya dola 900 milioni za Kimarekani mwishoni mwa wiki, mabosi wa sinema wanasubiri kuona kiwango cha fedha kitakachopatikana katika filamu zenye hadithi za ngono na dawa za kulevya kama vile filamu ya "I'm Still Standing".
 
Ngono, dawa za kulevya na Elton John -
Tofauti na filamu ya mwanamuziki nyota Freddie Mercury, ambayo ilijikita zaidi katika maisha yake binafsi, sinema ya Elton John inamuonyesha akijivunia maisha yasiyopendeza.
Elton -- ambaye amekuwa mkweli kuhusu jinsi anavyotaabika katika masuala ya jinsia, dawa za kulevya na pombe-- alihusika sana katika filamu hiyo ambayo imetayarishwa na 'mumewe', David Furnish.
"Nadhani tungevutia zaidi studio na kwa gharama kubwa zaidi kama tungetaka kutengeneza filamu inayoonyesha maisha safi ya Elton," alisema Furnish.
"Lakini hilo halikumvutia Elton," aliongeza. "Maisha yake yalikuwa na nyakati za ajabu na pia yasiyo safi. Tulitaka kuwa wakweli kuhusu mambo hayo."