Tanesco yatwaa ubingwa wa jumla mashindano ya Shimmuta

Muktasari:

Mashindano hayo yanafanyika jijini Mwanza yakishirikisha timu 16 katika michezo mbalimbali ikiwamo soka, wavu, kikapu na kuvuta kamba.

Mwanza.Tanesco imetwaa makombe 11 na kushinda ushindi wa jumla katika mashindano ya Michezo ya Mashirika ya Umma, Taasisi na Kampuni Binafsi za Tanzania (SHIMMUTA) yaliyomalizika Jijini Mwanza.

Katika fainali ya mchezo wa soka Tanesco ilifanikiwa kutwaa ubingwa huo baada ya kuichapa TRA kwa penalti 5-4 baada ya kumaliza dakika 90 kwa sare 1-1.

Tanesco imetwaa ubingwa huo wa soka ikiweka rekodi ya kushinda mechi zake zote tangu hatua ya awali hadi katika fainali hiyo.

Mbali ya kutwaa ubingwa wa soka, pia Tanesco imeondoka na mataji katika mpira wa pete, wavu wanaume na wanawake na mpira wa kikapu wanaume.

Kwa upande wa mpira wa kikapu wanawake Tanesco imeshika nafasi ya pili.

Katika mchezo wa Karata, Joseph Mzee kutoka Tanesco alitwaa ubingwa huo, huku Rukia Wandwi akishika nafasi ya pili katika Darts wanawake na Anna Msangi alipata nafasi ya pili katika mchezo wa pool table wanawake.