Tigana kuzika Msasani

MWILI wa nyota wa zamani wa kimataifa wa Tanzania, Ally Yusuf 'Tigana' aliyefariki dunia jana mchana, unatarajiwa kuzikwa saa 10 jioni kwenye makaburi ya Msasani, jijini Dar es Salaam.
Tigana aliyezichezea klabu mbalimbali ndani na nje ya nchi zikiwamo Pan Africans, Yanga, Simba na Cadets ya Mauritius alikumbwa na mauti katika hospitali ya Amana baada ya kuugua ghafla alipoenda kumtembelea mkewe aliyelazwa hospitalini hapo kabla hali yake kubadilika akiwa nyumbani na kuwahishwa hapo akilalamika tumbo linamsyumbua kiasi cha akitapika na kuharisha.
Mmoja wa rafiki wa karibu wa familia ya marehemu na aliyewahi kucheza naye enzi za uhai wake, Mwanamtwa Kihwelu alisema, mazishi ya Tigana aliyezaliwan mwaka 1970 jijini Dar es Salaam utazikwa saa 10 jioni Msasani.
Tigana aliyepachikwa jina hilo akifananishwa na nyota wa zamani wa Ufaransa, Jean Pierre Tigana, aliyecheza soka ya ushindani kwa kipindi cha miaka 17 kuanzia mwaka 1975- 1991,  alijiunga na Yanga mwaka 1994 na kukaa nayo hadi mwaka 1997 alipotimkia Mauritius alikocheza hadi 2000 kabla ya kurejea nchini na kujiunga na Simba kwa msimu mmoja kisha kujiunga Yanga 2001-2004.