Utata wa Kanda, Mazembe yambakisha Msimbazi

BAADA ya sintofahamu juu ya hatma ya nyota matata anayekipiga Simba kwa mkopo kutoka TP Mazembe ya Dr Congo, Deo Kanda, kila kitu kwa sasa kinaelezwa kipo freshi na jamaa ataendelea kukinukisha Msimbazi.
Wakala wa mshambuliaji huyo kutoka Kongo, anayeitwa Rashid Hassan  amesema, mpango mchezaji huyo kuendelea na Simba umekaa vizuri.
Rashid ambaye ndiye aliyemleta Kanda Msimbazi msimu huu,  amesema mipango ya TP Mazembe kumwachia Kanda inakwenda vizuri na kwamba kuna matumaini makubwa ya kusalia kikosini hapo, licha ya awali kuelezwa huenda angerudishwa TP ama kusajiliwa Jangwani.
"Hakuna tatizo lolote juu ya Kanda na Simba nimeshaweka kila kitu sawa na hivi sasa jambo hilo ndio nalishughulikia, "  amesema wakala huyo.
Amedokeza kuna mpango wa kumalizana kabisa na TP Mazembe ili acheze Simba hadi atakapostaafu au apewe muda mwingine kama alivyotolewa awali kwa mkopo.
Tangu ajiunge na Simba kwa mkopo kwa mkataba wa mwaka mmoja mwanzoni mwa msimu huu Kanda amekuwa akifanya vizuri hata kuwashawishi watani wao Yanga wamuwanie, akiwa amefunga mpaka sasa mabao saba katika Ligi Kuu Bara.
Nyota huo aliyecheza fainali ya Klabu Bingwa ya Dunia mwaka 2010 dhidi ya Inter Milan ya Kocha Rafa Benitez na kufumuliwa mabao 3-0, amesema angependakucheza Simba kwa kipindi kirefu kwa sababu anafurahia maisha ya hapa.
Kanda pia alikuwa kwenye kikosi kilichotwaa Ligi ya Mabingwa Afrika mwaka 2010 akiwa na TP Mazembe kuonyesha alivyo mzoefu wa soka la kimataifa.