Vanessa amuachia msala Jux

NYOTA wa muziki wa kizazi kipya nchini, Juma Jux amesema kuachana na Vanessa Mdee kumemuachia msala, akipoteza marafiki wengi kitu ambacho anakichukua kama changamoto.
Wawili hao walikuwa ni wapenzi wa muda mrefu na kila mmoja amekiri kuachana na mwenzake, huku Jux akitambulisha mahusiano yake mapya.
Akizungumza na Mwanaspoti, Jux alisema tangu ameachana na mwanadada huyo amekuwa akikwepwa na marafiki zake wengi huku akiweka wazi kuwa wengi wao wanahofia kuwa karibu naye kwa kuonekana wapo upande wake.
"Huwezi kuamini kuna watu siku hizi wananikwepa siwezi kuwataja ila ukweli ndio huo kwani walikuwa rafiki zetu wote mimi na Vanessa hivyo wanaogopa wakiwa pamoja na mimi wataonekana wapo upande wangu," alisema na kuongeza kuwa;
"Wengine hata kupiga picha nami wanaogopa hawataki kuonekana wapo upande gani natengwa nazani sio kwangu tu hata Vanessa yanamkuta hayo," amesema.
"Nina imani hili pia litapita kwani ata mwanzo wa mimi na Vanessa kuna watu waliokuwa wanajua nipo na Jack walijitenga, ila baadae wakarudi hivyo nachukua kama changamoto," amesema.