Wazee Stars waongeza mzuka mazoezini

Muktasari:

  • Ujio wa wachezaji hao uliongozwa na mshambuliaji Peter Tino ambaye alifunga bao la kusawazisha nchini Zambia katika sare ya bao 1-1 ambalo liliivusha Stars kwa ushindi wa jumla wa mabao 2-1 kufuatia ushindi wa bao 1-0 nyumbani Dar es Salaam.

Nyota wa zamani wa timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' walioiongoza kufuzu Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON) wameibuka katika mazoezi ya timu hiyo yanayoendelea kwenye Uwanja wa Taifa jioni hii kwa ajili ya kuwapa hamasa wachezaji kuelekea mchezo wa kuwania kufuzu fainali hizo dhidi ya Uganda Jumapili.

Ujio wa wachezaji hao uliongozwa na mshambuliaji Peter Tino ambaye alifunga bao la kusawazisha nchini Zambia katika sare ya bao 1-1 ambalo liliivusha Stars kwa ushindi wa jumla wa mabao 2-1 kufuatia ushindi wa bao 1-0 nyumbani Dar es Salaam.

Mbali na Tino, wengine waliofika kwenye Uwanja wa Taifa ni Iddi Pazi, Hussein Ngulungu, Leopard Tasso, Omary Hussein 'Keegan' na wengineo.

Akizungumzia ziara hiyo ya ghafla, Tino alisema inalenga kuwahamasisha wachezaji kwa ajili ya mechi hiyo dhidi ya Uganda "Kikubwa tumefika hapa kuwapa morali wachezaji wafahamu umuhimu wa kufuzu Fainali za Mataifa ya Afrika," alisema Tino.