Yanga yaikaribisha AS Roma katika ulimwengu wa Kiswahili Tanzania

Dar es Salaam. Klabu ya Yanga imekuwa timu ya kwanza kuikaribisha AS Roma katika ulimwengu wa lugha ya Kiswahili kwa kusema wako pamoja na kuwakaribisha Tanzania.

AS Roma ya Italia imekuwa klabu ya kwanza barani Ulaya kuanzisha ukurasa wa mtandao wa kijamii wa Twitter utakuwa ukiendeshwa kwa lugha ya Kiswahili.

Ukurasa huo, ulifunguliwa Jumatano kwa lengo la  kuwafikia kwa wepesi wapenda soka wa ukanda wa  Afrika Mashariki ambako kwa asilimia kubwa wamekuwa wakitumia lugha ya Kiswahili katika mawasiliano.

Baada ya kuuzindua waliandika maneno haya,"Ahsante sana kwa upendo na ushirikiano ambao mmetuonesha tangu tumezindua ukurasa huu rasmi.

"Ni dhahiri kwamba kwa pamoja tutaendelea kushirikiana na kufurahia pamoja hapa hapa kwa lugha ya Kiswahili. Endelea kuja kwa wingi zaidi."

Kwa mtazamo mwingine AS Roma, wanaonekana kulenga kujiongezea mashabiki ukanda wa Afrika  Mashariki ambao umekuwa ukizifuatilia kwa ukaribu klabu za Ligi Kuu England.