VIDEO: Yanga yatua Mwanza, Zahera uteja kwa Mbao basi

Muktasari:

  • Yanga imetua Mwanza asubuhi na leo jioni inatarajia kufanya mazoezi kujiandaa na mchezo wa Jumatano dhidi ya Mbao FC.

Mwanza. Kikosi cha Yanga kimetua jijini Mwanza asubuhi ya leo huku kocha Mwinyi Zahera akiwa na lengo moja tu la kufuta uteja dhidi ya Mbao keshokutwa Jumatano kwenye Uwanja wa Kirumba.

Yanga wametua Mwanza wakiwa na kumbukumbu ya kupoteza mchezo wake uliopita dhidi ya watani zao Simba kwa bao 1-0, kinawakabili Mbao FC huku kikiwa na rekodi mbaya ya kutopata ushindi katika uwanja wa CCM Kirumba Mwanza.

Akizungumza baada ya kutua uwanja ndege jijini hapa, Kocha Mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera amesema hawachezi kwa rekodi badala yake wanakuja kupambana kusaka ushindi.

Amesema ikiwa ni mechi yake ya kwanza dhidi ya Mbao kwenye Uwanja wa Kirumba, anakuja kuvunja rekodi kwani kikosi chake kipo fiti na hakuna majeruhi yeyote ambaye atakosa mpambano huo na kuwaomba mashabiki kujitokeza kwa wingi kushangilia timu hiyo.

Timu hizo zimekutana mechi tatu, ikiwa mbili za ligi Kuu na moja ya Kombe la Shirikisho ambapo Yanga walipoteza zote hivyo kufanya mechi ya Jumatano kuwa ya kuvunja au kuendeleza rekodi.