Yanga yavunja mwiko kwa Mbao FC ikishinda mabao 2-1

Muktasari:

Ushindi huo unawafanya vijana hao wa Jangwani kufikisha alama 61 na kuendelea kujiimarisha kileleni kwenye msimamo wa Ligi Kuu.

Mwanza. Timu ya Yanga imeibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya wenyeji wao Mbao FC kwenye mchezo wa Ligi Kuu kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Mabao ya Yanga yaliwekwa wavuni na Haritier Makambo pamoja na Amisi Tambwe ambapo mabao yote yalifungwa katika kipindi cha pili.

Ushindi huo unawafanya vijana hao wa Jangwani kufikisha alama 61 na kuendelea kujiimarisha kileleni kwenye msimamo wa Ligi Kuu.

Awali, dakika ya 45 kipindi cha kwanza straika wa Mbao Ndaki Robert aliipeleka timu yake mapumziko kibabe kutokana na bao murua alilofunga kwa kichwa akiunganisha mpira wa Amos Charles.

Pamoja na kwamba timu zote zilikuwa zikishambuliana kwa zamu,lakini umakini  wa Yanga katika eneo la mbele likiongozwa na Makambo na wakati mwingine walikosa mawasiliano kutokana na kushindwa kutumia vyema nafasi walizopata.

Hata kwa upande wa Mbao nao licha ya kutangulia kupata bao, lakini walistahili kwenda mapumziko hata na zaidi ya bao moja kwani nafasi walizopata walishindwa kuzitumia vyema haswa ya Pastory Athanas.

Jambo la kushangaza waamuzi hawakwenda vyumbani kupumzika baada ya mashabiki kiwarushia chupa za maji na kuwafanya kutulia kwa muda uwanjani na baadaye kufanikiwa kuondoka chini ya ulinzi wa Askali Polisi.