VIDEO: Yanga yazindua kampeni 'Twenzetu Ndola tukapindue meza kibabe'

Muktasari:

  • Yanga inakibarua kigumu kutafuta ushindi au sare ya mabao kuanzia mawili na kuendelea ili waweze kuing'oa Zesco katika mchezo wa marudiaono kusaka nafasi ya kutinga hatua ya Makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Dar es Salaam. Katika kuhakikisha wanapata ushindi mchezo wa marudiano wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Zesco ya Zambia, uongozi wa Yanga imezindua kampeni maalum ya kuhakikisha wanashinda katika mechi hiyo.
Akizungumza Jijini Dar es Salaam, leo Mwenyekiti wa Kamati ya hamasa ya Yanga, Sums Mwaitenda mbali na kuwashuru mashabiki waliojitokeza katika mchezo kwa kwanza wikiendi iliyopita amesema bado klabu yao ina nafasi ya kutinga hatua ya makundi.
Mwaitenda amesema baada ya kupata mashabiki wasiopungua 30000 katika mchezo wa kwanza sasa wanataka kuona hatua ya kwanza ni kuhakikisha mashabiki wengi wanasafiri kuelekea jijini Ndola nchini Zambia kuishangilia timu yao ya Yanga kuipa nguvu.
Alisema katika kufanikisha hilo wamezindua kauli mbiu itakayosema 'Twenzetu Ndola tukapindue meza kibabe' ambapo kupitia kauli hiyo wanaamini itawaamsha mashabiki wengi kujitokeza.
Aidha Mwaitenda alisema katika hamasa hiyo ya mashabiki pia kamati yao pamoja na wachezaji wa zamani kwa pamoja watakutana na wachezaji na timu yao nzima katika kuwapa morali ya kufanya vizuri katika mchezo huo.
Naye katibu wa kamati hiyo Deo Mutta alisema safari ya mashabiki hao kuelekea Ndola itakuwa na sura tofauti kwa makundi ambayo yataanzia ya Yale ya Nyanda za juu Kusini Iringa, Songwe, Njombe na Mbeya ambao safari yao itanzia Tunduma kuelekea Ndola huku gharama ikiwa Sh 110,000 kwa kwenda na kurudi.
Mutta alisema kwa mikoa mingine ya Dar es Salaam, Lindi, Mtwara na Pwani gharama za safari itakuwa ni Sh 200000 kwa kila kitu kasoro chakula na malazi.
Alisema kwa wanachama wenye hati ya kusafiria,hati ya chanjo gharama yao itakuwa ni Sh 150,000 ambapo wote watakaohitaji kwenda wanatakiwa kukamilisha malipo kabla ya Septemba 22,2019 huku safari ilitarajiwa kuanza Septemba 25.
Baada ya sare ya bao 1-1 wikiendi iliyopita Yanga itahitaji ushindi wowote au sare ya kuanzia mabao 2 na zaidi kuwang'oa Zesco ugenini  katika mchezo utakaopigwa Septemba 28 jijini Ndola,nchini Zambia.