Zahera aanika sababu za Yanga kuipiga Simba Taifa

Muktasari:

  • Yanga inatarajia kuwa mwenyeji katika mchezo huo unaotarajiwa kuchezwa saa kumi jioni katika uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaaam.

KOCHA Mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera amesema wanakila sababu kushinda katika mchezo wao wa kesho dhidi ya Simba kutokana na maandalizi waliyoyafanya ikiwa ni pamoja na ufiti walionao wachezaji wao.

Yanga inatarajia kuwa mwenyeji katika mchezo huo unaotarajiwa kuchezwa saa kumi jioni katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaaam.

Akizungumza Dar es Salaam leo, Zahera alisema nyota wake wote wako fiti mtiani alionao ni mmoja tu wa kuhakikisha anamchagua nani aanze na nani amuache kikubwa anachoshukuru ni nyota wake wote kuwa tayari kwaajili ya mchezo.

Alisema hautakuwa mchezo mwepesi kwao anaamini utakuwa mgumu lakini wamejipanga kwaajili ya ushindi utakuwa ni mchezo mzuri kwao na anaamini atawashangaza wengi.

"Tumetoka kucheza michezo mitatu ya ligi mfululizo tukiwa tunatafuta matokeo tumetumia masaa 32 naona kama ni maajabu sana katika soka tumetumia kilometa 2000 na naweza kusema mipango inayofanywa sio mizuri," alisema.

"Safari yetu tulikuwa na mipango ya kupata pointi tisa lakini tumepata tano nyingine nne tumeibiwa kwasababu kuna mabao tulishinda yamekataliwa lakini hatuna sababu ya kuzungumza sana tumefurahia pointi hizo tano," alisema.

Alitumia nafasi hiyo kuwaomba marefa kutumia sheria 17 za mpira kila mmoja ashinde kutokana na juhudi atakazozifanya uwanjani ili kuepusha mambo mengine ambayo hayatakuwa na maana viwanjani.