Kinachomfanya mpenzi wa Diamond asitaje jina la mwanaye chabainishwa

Muktasari:

Kupitia instalive, Tanasha Donna ambaye ni mpenzi wa msanii wa muziki nchini Tanzania, Diamond Platinumz amebainisha sababu ambazo zinamfanya asitaje jina la mwanae mtarajiwa.

 

Dar es Salaam. Tanasha Donna ambaye ni mpenzi wa msanii wa muziki wa kizazi kipya nchini Tanzania Diamond Platnumz amesema anaogopa kutaja jina la mwanaye mtarajiwa kwa sababu ya kuwaogopa watu wabaya wasije kumdhuru.

Ingawa amesisitiza kuwa anaamini Mungu lakini ni hatari kuweka hadharani jina la mwanaye kwa sasa.

Kupitia instalive, Tanasha anayetarajia kupata mtoto wa kiume na mpenzi wake Diamond, alikuwa akijibu maswali ya mashabiki zake.

Alipoulizwa kama wameshajadili jina la mtoto wao, amesema wamejadili lakini litabaki kuwa kichwani mwake na ni siri yake.

"Naogopa watu wabaya wasije kumdhuru mwanangu, siwezi kulitaja ila tumeshajadili na linajulikana," amesema Tanasha huku akionyesha ishara ya kupuliza kiganja kuashiria ushirikina.

Amefafanua jina la mtoto wake litakuwa la Kiislamu kwa sababu hata mtoto atakuwa ni dini hiyo pia.

Tanasha ambaye ni raia wa Kenya amewaeleza mashabiki wake kuwa atamfundisha mwanaye lugha tatu ambazo ni Kiswahili, Kiingereza na Kifaransa.