Akon asaini mkataba wa ujenzi wa mji wake

Muktasari:

Mwimbaji Akon, mwenye asili ya nchini Senegal ametiliana saini na kampuni ya Sapco kwa ajili ya kuanza ujenzi wa mji wake ‘Akon City’ ambao wakati wake watakuwa wakitumia sarafu yake iitwayo Akoin, ukiwa na majengo ya biashara, viwanja vya ndege na burudani.

Dar es Salaam. Msanii  miondoko ya Pop na R&B kutoka Marekani mwenye asili ya Senegal,  ametiliana saini  makubaliano ya hatua za ujenzi wa mji wake utakaoitwa Akon City ambao utajengwa nchini kwao Senegal.

Kupitia ukurasa wake wa Instagram staa huyo ameweka picha ikimuonyesha akitiliana saini  na kampuni ya utalii iitwayo  SAPCO kwa ajili ya ujenzi wa mji huo utakaokuwa na kilomita 120 kutoka ulipo mji mkuu wa Senegal, Dakar.

Mji huo utajengwa katika eneo la ekari 2,000 za ardhi zilizotolewa na rais wa Senegal  utakuwa na kila kitu ikiwamo viwanja cha ndege, viwanja vya burudani, majengo ya biashara.

Akon aliwahi kunukuliwa akisema mji huo utakamilika kujengwa mwaka 2025 na wakazi wake watakuwa wakitumia sarafu ya kidijitali itakayoitwa ‘Akoin’, katika biashara.

Mitandao mbalimbali inaeleza mji huo utakuwa kama ule unaoonekana katika mji wa Wakanda unaoonekana katika filamu ya Black Panthe, ukitumia nishati ya sola badala ya umeme wa kawaida.