Alicia Keys aingia studio kuimba singeli

Muktasari:

Msanii wa Marekani, Alicia Keys ameingia studio kufanya remix ya wimbo wa singeli wa Wanga wa msanii wa Tanzania, Meja Kunta aliyemshirikisha Lavalava wa lebo ya WCB.

Dar es Salaam. Msanii wa Marekani, Alicia Keys ameingia studio kufanya remix ya wimbo wa singeli wa Wanga wa msanii wa Tanzania, Meja Kunta aliyemshirikisha Lavalava wa lebo ya WCB.

Alicia anafanya hivyo siku chache baada ya mumewe,  Swizz Beatz ambaye ni mtayarishaji wa muziki maarufu nchini Marekani kuweka vipande vya wimbo huo katika ukurasa wa mtandao wake wa kijamii wa Instagram.

Ni kama Swizz Beatz aliupenda wimbo huo na kuamua kumuingiza mkewe studio kuufanyia remix.

Picha za video zilizopo katika mtandao wa kijamii wa Instagram zinamuonyesha Alicia Keys aliyevaa koti la rangi ya kaki, na fulana akicheza wimbo huo kwa madaha kama Mtanzania aliyepo katikati ya jiji la Dar es Salaam.

Chini ya video hiyo aliyoitupia katika ukurasa wake wa Instagram, Alicia Keys amesema “Big Zone”.

Meneja wa WCB, Hamis Tale maarufu Babu Tale amesema, “ni makubaliano kati yetu wameupenda wimbo huo na wakaomba kuufanyia remix, tukatae sisi nani.”