Fiesta Dar es Salaam sasa Desemba 22, kuongozwa na Alikiba

Muktasari:

  • Tamasha la Tigo Fiesta kufanyika Desemba 22 mwaka huu viwanja vya posta Kijitonyama vilivyopo jijini Dar es Salaam likiongozwa na mfalme wa Bongo fleva Alikiba.

Hatimaye kilele cha tamasha la Tigo Fiesta kufanyika Desemba 22 mwaka huu ikiwa ni takribani mwezi mmoja tangu liahirishwe na waandaaji wake saa chache kabla ya kufanyika.

Tamasha hilo lililopaswa kufikia tamati Novemba 24 baada ya kuzunguka kwa miezi mitatu katika mikoa 14, liliahirishwa baada ya kudaiwa kuwa eneo lililopangwa kufanyika lingeleta usumbufu kwa wagonjwa na kuwashauri waandaaji watumie viwanja vya Tanganyika Packers vilivyopo Kawe jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Kinondoni, Aaron Kagulumjuli aliiambia Mwananchi kuwa tamasha hilo lingesababisha usumbufu kwa wagonjwa ingawa hakutaja jina la hospitali husika.

“Tumelizuia tamasha kufanyika hapo kwani uhai wa watu ni muhimu kuliko hicho kinachotaka kufanyika. Jana tu walipokuwa wakitangaza hapo Leaders maeneo ya karibu kuna hospitali na watu wawili walizimia, sasa hatuwezi kuruhusu furaha ya watu wengi ikawa majonzi kwa wengine,” alisema.

Kupitia ukurasa wa Instagram wa Alikiba anayetamba na wimbo Mvumo wa Radi alisema kuwa atawaachia mashabiki zake nyimbo za kufungia mwaka huku akisogeza mbele tarehe ya shoo yake ambayo ingefanyika katika ukumbi ulioko katika hoteli ya Serena jijini Dar Es Salaam ili kushiriki Tigo Fiesta.

“Kuna mabadiliko ya tarehe ya shoo yangu na Mama Yvonne Chaka Chaka pamoja na King Of Best Melodie Christian Bella, siku hiyo nitapanda jukwaani na wanangu wa King Music Records. “