Chid Benz amjia juu Harmonize

Muktasari:

Msanii  Chid Benz amemjia juu  Harmonize baada ya kumtaja katika orodha itakayomsindikiza kwenye tamasha lake litakalofanyika viwanja vya Mwembe Yanga, Dar es Salaam bila kuwasiliana naye.

Dar es Salaam. Zikiwa zimebaki siku mbili kabla ya kufanyika kwa tamasha la ‘Jipoze na Twist Tour’ la msanii Harmonize hali imekuwa sio shwari kati yake na msanii mwenzake nchini Tanzania, Chid Benz.

Hilo limejitokeza jana Jumanne Januari 28, 2020 baada ya Harmonize kuweka orodha ya wasanii watakaomsindikiza katika tamasha hilo litakalofanyika Februari 1, 2020 uwanja wa Mwembe Yanga, Dar es Salaam uliopo Tandika huku Chid Benz akitajwa kuwa mmojawapo.

Hata hivyo, tangazo hilo lilipokelewa ndivyo sivyo na Chid ambaye kupitia ukurasa wake kwenye mtandao wa Instagram aliandika, ‘Sikia mdogo wangu hii ni kazi, usinichukulie poa, hivi unatangaza kazi bila kunijulisha chochote wala kuongea na mimi.”

“Namba yangu ni.., heshima ifuate mkondo wake. Sijakataa wala hatujakataa ila sijui hata malipo yakoje, no hard filn, sipo kwenye hiyo show.”

“Sidhani kama popote ulipo huwezi kufanya mawasiliano kama kweli ni kazi piga simu,” aliandika Chid Benz ambaye jina lake halisi ni Rashid Makwiro.

Tayari Harmonize amechukua hatua ya kuondoa jina la msanii huyo katika orodha yake hiyo iliyokuwa na wasanii tisa sasa wamebaki wanane.

Wasanii hao waliobaki  ni pamoja na Amber Lulu, Juma Nature, Mimi Mars, Young Lunya, Baranaba, Sholo Mwamba, Whozu na Country Boy.