Daz Baba: Nina watoto saba, sijapata mwanamke wa kumuoa

Muktasari:

  • Msanii Daz Baba ameanika sababu za kutooa hadi leo licha ya kuwa an watoto saba kuwa ni kukosa mke anayemfaa

Dar es Salaam. Msanii  Daz Baba amesema licha ya kuwa na watoto saba kutoka kwa mama tofauti lakini hajapata mwanamke mwenye sifa za kumuoa.

Akizungumza na Mwananchi hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Daz Baba aliyewahi kutamba na wimbo 'Umbo namba 8' amesema hataki kuoa kwa kufuata mkumbo kwa sababu ndoa ni jambo la kudumu.

“Sitaki kuwa mfano mbaya kwa watoto wangu, yaani niwe naoa na kuacha, ndiyo maana nimeamua kutulia nitafute mke atakayenifaa kwa bahati mbaya hadi leo sijampata, ”amesema

Amesema wasanii au mastaa wengi huoa kwa kufuata mkumbo na matokeo yake ndoa zao huvunjika ndani ya muda mfupi.

“Waliooa wanastahili heshima, kupata mke ni kazi tofauti na kupata mwanamke,” amesema huku anacheka.