Diamond Platnumz atajwa na CNN orodha ya wasanii bora 10 Afrika

Muktasari:

Shirika la Utangazaji CNN limetaja wanamuziki bora 10  barani Afrika, akiwemo msanii wa Tanzania, Diamond Platnumz.

Dar es Salaam. Shirika la Utangazaji CNN limetaja wanamuziki bora 10  barani Afrika, akiwemo msanii wa Tanzania, Diamond Platnumz.

Orodha hiyo inamfanya Diamond kuwa msanii pekee kutoka Afrika Mashariki kuingia katika orodha hiyo ya wasanii wanaofanya vizuri katika muziki.

Wengine waliotajwa ni Burna Boy wa Nigeria ambaye pia ameteuliwa katika tuzo za Grammy zitakazofanyika Januari  2020 pamoja na Yemi Alade, Tiwa Savage na Wizkid wote wa nchi hiyo.

Mtunzi, mwanaharakati na mshindi wa tuzo ya Grammy kutoka nchini Benin,  Angelique Kidjo pia amejumuishwa katika orodha hiyo.

Pia wapo waimbaji wa Afrika Kusini, Sho Madjozi, Busiswa Gqulu ambaye pia ni mwandishi wa nyimbo na mshairi, rapa wa Zambia,  Mwila Musonda  maarufu Slapdee.

Diamond ambaye ameingia katika tasnia ya muziki miaka 10 iliyopita amekuwa na mafanikio makubwa.