Teknolojia: Iphone zijazo zitakuwa na bluetooth mbili

Teknolojia inazidi kutuacha hatua nyingi mbele. Mpaka sasa umetumia iPhone ipi na ipi? Je, umeweza kutumia kila ulichowekewa katika simu yako au umebaki kutuma meseji, kupiga simu na kujipiga selfie?

Mbali na kuwa na vitu vingi unavyoweza kufanya katika simu yako, watengenezaji wanatarajia kuongeza udambwi udambwi mwingine katika matoleo mapya ya simu hizo.

Mojawapo ya maujanja yatakayoongezwa ni Bluetooth itakayomwezesha mtumiaji kujiunga na vifaa viwili vya mawasiliano kwa wakati mmoja kama vile vya kucheza muziki.

Kingine kitakachoongezwa ni uwezo wa kuchaji simu bila kuweka kwenye soketi pamoja na ukubwa wa betri kwa asilimia 10 mpaka 15.

Maana yake ni kwamba pamoja na kuongezwa vikorombwezo, simu itakuwa na uwezo wa kukaa na chaji mara 15 zaidi ya matoleo ya mwisho.