Kilichomkondesha Wema Sepetu hiki hapa

Muktasari:

  • Meneja wa mrembo wa Tanzania mwaka 2006,  Wema Sepetu ameweka bayana kilichomfanya mrembo huyo kukonda ni kutokana na mazoezi si kukatwa utumbo.

Dar es Salaam. Baada ya kuzagaa kwa habari kwamba kupungua mwili kwa mrembo Wema Sepetu, kumetokana na kukatwa utumbo, meneja wake amefunguka na kuanika ukweli.

Katika mahojiano na Mwananchi leo Jumatatu Februari 4, 2019 meneja huyo, Neema Ndepanya amesema Wema hajakatwa utumbo bali amekuwa akifanya mazoezi kwa wingi na kupunguza kiwango cha kula.

Neema amesema mazoezi hayo, Wema ameyafanya kwa takriban  miezi sita sasa na amekuwa ni mtu ambaye anafuata masharti yote anayoelekezwa na mtaalamu wa mazoezi

"Watu waache kuongea mambo ya kutunga, Wema hajakatwa utumbo jamani ni mazoezi tu ndiyo yamemfanya vile na kilichomsaidia zaidi amekuwa mtu wa kufuata masharti.

"Nampongeza sana kwani nilianza naye mazoezi, lakini mimi masharti mengine yalinishinda kwa ukweli ndio maana mimi bado nimenenepeana, mwenzangu anazidi kukonda," amesema meneja hyo.

Amesema kutokana na kufuata masharti hayo, Wema amejikuta akipunguza kilo zaidi ya 26 kwani wakati anaanza alikuwa na kilio 96 kiwango ambacho ni kikubwa sio kazi rahisi kama mtu anavyofikiria.

Kuhusu adhabu yake, amesema inaelekea ukingoni kwani maagizo mengi aliyopewa anaelekea kuyakamilisha na kwamba ni moja ya mambo ambayo yamekuwa yakimuumiza.

Hata hivyo, meneja huyo anabainisha kwamba pamoja na kumtaka Wema apumzike kufanya na kazi zingine kwa muda kutokana na lililompata, kuna kampuni nyingi zinamfuata kutaka kufanya naye kazi na hadi sasa zimejitokeza sio chini ya tatu  kubwa.

"Jamani aliyepewa kapewa, Wema ana nyota yake tu hilo lazima watu tukubali yaani ni 'Heaven Sent' huyu mtu maana ingekuwa mtu mwingine kwa alilolipitia ungekuta kasahaulika," amesema Neema.

Oktoba 2018, Bodi ya Filamu ilimfungia Wema kutojihusisha na kazi za filamu baada ya kusambaza picha katika ukurasa wake wa Instagram zilizomuonyesha akiwa faragha na mwanaume.