Kumbe Julai 7 ya Diamond ipo hivi

Muktasari:

Hamis Tale ambaye ni meneja wa msanii wa Tanzania, Diamond ametoboa siri kwamba mama  na mchumba wa msanii huyo, Tanasha wamezaliwa tarehe na mwezi mmoja ambapo Julai 7, 2019 kutafanyika tukio ambalo hajaliweka wazi litakuwa lipi.

Dar es Salaam. Kama ni mfuatiliaji wa masuala ya burudani ni wazi kwamba utakuwa unasubiri Julai 7, mwaka 2019 nini kitatokea kwa msanii wa Tanzania, Diamond Platnumz.

Msanii huyu ambaye jina lake halisi ni Naseeb Abdul, akiwa katika mkutano na waandishi wa habari wiki iliyopita alitangaza msimu wa pili wa tamasha la wasafi sambamba na tukio kubwa Julai 7,2019, alilodai litafanyikia maeneo ya Mwenge, Dar es salaam Tanzania.

Mwananchi leo Jumanne, Julai 2,2019  lilitafuta undani wa tukio hilo ambapo Meneja wake Hamis Taletale maarufu ‘Babu Tale’ amezungumzia suala hilo.

“Ni kweli siku hiyo kutakuwa na tukio kubwa kwa msanii wetu huyo (Diamond), ambapo ni siku ya kuzaliwa kwa mama yake Sandra na mchumba wake Tanasha Donna ambao wote wamezaliwa Julai 7 kasoro miaka tofauti.”

“Pamoja na kwamba ni siku ya kuzaliwa kwa wapendwa wake hao,  lakini pia lolote linaweza kutokea ikiwemo ndoa ambayo mashabiki wake wengi wanahisi hivyo ila tusubiri muda ndio utakaoongea,” amesema Babu Tale.