Lulu kuitumia ‘Valetine Day’ kuuza nguo zake

Muktasari:

 

  • Msanii Lulu amebadilisha uamuzi wake wa kuzigawa nguo zake bure na sasa ataziuza huku fedha itakayopatikana, itasaidia watu wenye mahitaji maalumu

Dar es Salaam. Msanii wa filamu nchini Tanzania, Elizabeth Michael maarufu Lulu ametangaza rasmi siku ya kuuza nguo zake anazovaa.

Hatua hiyo inakuja baada ya wiki moja iliyopita kutangaza kuzigawa nguo hizo ambazo aliwahi kuzivaa na watu kuzipenda.

Hata hivyo, leo Jumatano Juanuari 23,2019 Lulu katika ukurasa wake wa mtandao wa Instagram, ameeleza kubadili uamuzi wa kuzigawa nguo hizo badala yake, ataziuza siku ya sikukuu ya wapendao ‘Valetine Day’.

Katika tangazo hilo Lulu ameandika: “Wakati wengine tumepata fursa ya kuwa na furaha kwa vile tulivyonavyo, kuna baadhi ya wenzetu wamekosa nafasi hiyo na huu ni mpango wa Mungu.

“Kuelekea siku ya wapendanao Februari 14, nimeamua kuuza sehemu ya nguo zangu ambazo yawezekana umeshawahi kuziona au haujaziona.

“Pesa yote itakayopatikana kupitia mauzo haya itaenda kusaidia vitu au watu wenye uhitaji katika jamii, Please Join me to Save My Valentine (Tafadhali ungana na mimi kuokoa niwapendao)’.