Mahusiano ya Diamond, Tanasha njia panda

Muktasari:

Familia ya msanii wa Tanzania, Diamond Platnumz imepata kigugumizi cha kueleza ukweli kuhusiana na kuvunjika kwa mahusiano kati ya msanii huyo na mpenzi wake Tanasha Donna.

Dar es Salaam. Wakati kukiwa na tetesi za Diamond kuachana na mpenzi wake Tanasha Donna, bado taarifa hizo zimeendelea kuwa siri kwa familia.
Tetesi za kuachana kwa wawili hao wanaotesa na wimbo wa 'gere' kwa sasa zilianza juzi katika mitandao ya kijamii baada ya Tanasha kwa nyakati tofauti kuweka ujumbe mbalimbali uliotafsiriwa kuwa ni vijembe kwa Diamond.
Pia, amekuwa akifuata baadhi ya picha kwenye ukurasa  wake zinazomuhusisha Diamond ikiwemo ile ya nyimbo yake mpya ya 'Jeje' aliyoiachia wiki iliyopita.
“Having a clean heart is Priceless because it’s so damn valuable that not even money can match up to its standards” aliandika Tanasha kwenye mtandao wa Instagram ikiwa na maana ya kuwa na moyo safi hakuna bei kwa sababu ni muhimu sana hata pesa haziwezi kulingana na viwango vyake, kauli ambayo ilianza kutafsiriwa kama vijembe kwa mwenza wake huyo.
Watu wa mitandao wamekuwa wakitafsiri hatua hiyo na maneno hayo ambayo amekuwa akiyaandika kama tayari Tanasha kaamua kuachana na Diamond ambaye walijaliwa kupata naye mtoto mmoja.
Kama vile haitoshi Tanasha ambaye mbali ya kuwa mwanamuziki ni video vixen na mtangazaji nchini Kenya, amekata mawasiliano na mama na dada yake Diamond kwenye ukurasa wake wa Instagram ambapo mtu ukiingia humo inasomeka  'unfollow' na 'block'.
Pia leo ameongeza idadi ya watu alioamua kukata nao mawasilano wengi wakiwa wale walio karibu na Diamond, wakiwemo wasanii wa lebo ya WCB. Kati ya hao wapo wasanii wa Bongofleva, Mbosso, Queen Darleen na Ray Vanny.
Hata hivyo, Mwananchi ilimtafuta Dada wa Diamond, Esma Platnumz ili kupata ukweli kuhusiana na jambo hilo ambalo kwa siku mbili hizi limekuwa gumzo katika mitandao ya kijamii
Katika majibu yake alijibu kwa kifupi “mimi sijui kwanza nimelala saa hizi” kisha akakata simu.