Mama wa Harmonize alivyopanda jukwaani kuimba na kijana wake

Muktasari:

Harmonize ameonyesha kile kilichokuwa kikisubiriwa na wengi kwa kujaza uwanja wa Kassim Majaliwa nyomi la watu licha ya kuwa na kiingilio cha Sh10,000, huku akimpandisha mama yake jukwaani ambaye aliwaimbisha mashabiki wimbo wake ‘Atarudi’

Dar es Salaam. Mtoto wa nyoka ni nyoka, ndicho ninachoweza kusema mara baada ya mama mzazi wa Harmonize kupanda jukwaani na kuimba wimbo wa kijana wake unaoitwa ‘atarudi.’

Mama huyo alipanda katika jukwaa alilofanya shoo Harmonize jana usiku Jumanne Desemba 31, 2019 kwenye viwanja vya Kassim Majaliwa wilayani Tandahimba mkoani Mtwara nchini Tanzania.

Hii ni shoo ya kwanza kubwa kwa Harmonize kuifanya akiwa nje ya lebo ya WCB na kukusanya maelfu ya mashabiki.

Akiwa jukwaani mama wa nyota huyo maarufu Konde Boy aliimba wimbo wa ‘Atarudi’, ulioimbwa na Harmonize , huku akisaidiwa na play back.

Jambo la kufurahisha mwanamama huyo ni kama alifanya mazoezi kwani alikuwa akiimba shairi na ikifika eneo la kiitikio alikuwa akiweka kipaza sauti kwa mashabiki waliofurika katika viwanja hivyo ambao walikuwa wakimsaidia kuitikia.

Akiwa amevaa gauni lenye mchanganyiko wa rangi ya pinki na nyeupe maarufu dashdash mama huyo alikuwa akiimba bila wasiwasi huku akinesa muda wote.