Zuchu msanii mpya WCB

Muktasari:

Zuchu, mtoto wa malkia wa taarab nchini Tanzania, Khadija Kopa ndio msanii mpya katika lebo ya WCB inayoongozwa na Diamond Platnumz.

Dar es Salaam. Zuchu, mtoto wa malkia wa taarab nchini Tanzania, Khadija Kopa ndio msanii mpya katika lebo ya WCB inayoongozwa na Diamond Platnumz.

Zuchu ametambulishwa jana Jumatano Aprili 8, 2020 na Diamond ambaye ni mkurugenzi wa lebo hiyo na kufanya idadi ya wasanii wa WCB kufikia sita.

Unaweza kusema Zuchu ametambulishwa rasmi kwa  kuwa alikuwa katika lebo hiyo tangu mwaka 2018.

Amewahi kushiriki shindano ya kusaka vipaji vya muziki  barani Afrika mwaka 2016 liitwalo  Tecno Own The Stage ambalo pia msanii Faustina Charles maarufu Nandy naye alishiriki na kupata Sh36 milioni baada ya kuwa mshindi wa  pili.

Mshindi wa shindano hilo alikuwa Shapeera wa Nigeria aliyejizolea kitita cha Dola 25,000.

Baadhi ya nyimbo ambazo Zuchu ameshirikishwa ni pamoja na ule wa Superwoman uliowahusisha wasanii mbalimbali wa kike nchini Tanzania ulioimbwa maalum kwa ajili ya kusherehekea siku ya wanawake duniani.

Zuchu amerudia nyimbo za msanii Mbosso, zikiwemo Nadekezwa na Maajabu na mara kadhaa ameshiriki kutengeneza matangazo mbalimbali ya redio ya Wasafi.