Mvua yasogeza mbele tamasha la Wasafi Dar es Salaam

Muktasari:

Kufuatia Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kutoa tahadhari ya uwapo kwa mvua kwa siku tano mfululizo, uongozi wa Wasafi umesogeza mbele tamasha lililokuwa lifanyike kesho Jumamosi jijini Dar es Salaam na hatima ya kujua linafanyika lini itajukana Jumatatu ya Oktoba 21, 2019.

Dar es Salaam. Tamasha la Wasafi lililokuwa lifanyike kesho Jumamosi Oktoba 19, 2019 kwenye viwanja vya Posta Kijitonyama jijini Dar es Salaam limesogezwa mbele.

Akizungumza na Mwananchi leo Ijumaa Oktoba 18, 2019  meneja wa lebo ya Wasafi ambayo ndiyo waandaaji wa tamasha hilo, Hamisi Tale maarufu Babu Tale amesema wamelisogeza mbele kutokana na tahadhari iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA) kuhusu uwapo wa mvua kuanzia Oktoba 18 hadi 22,2019.

“Tunaweza kufanya tamasha likatutokea puani, ndiyo maana ya kuwapo kwa mamlaka kama hizo, zinapotoa tahadhari tunazichukua na kuzifanyia kazi.”

“Tumelisogeza mbele na taarifa rasmi kujua linafanyika lini tutatangaza Jumatatu,” amesema Tale.