VIDEO: Mzee Yusufu ‘Narudi mjini’ gumzo kila kona

Muktasari:

Mzee Yusufu ameshtua watu leo baada ya kuandika ujumbe uliotafsiriwa kuwa huenda anataka kurudi katika muziki upya.

Dar es Salaam.‘Narudi mjini’. Hayo ndio maneno aliyoandika Alhaji Mzee Yusufu katika ukurasa wake wa mtandao wa Instagram, na kuzua maswali.

Maneno hayo ya Alhaji Mzee Yusufu aliyaandika leo Alhamisi Machi 12, 2020 jambo ambayo kila mtu kaitafsiri kwa namna yake.

Mzee Yusufu ambaye alikuwa mtunzi, mwimbaji na mpiga kinanda, mwaka 2016 alitangaza kuachana na muziki na kuingia kwenye masuala ya kufundisha dini na kutoa dawa kabla ya kwenda kuhiji Makka na jina lake hapo ndipo lilipobadilika na kuanza kuitwa Alhaji.

Akiwa kwenye muziki huo alitesa na nyimbo mbalimbali ikiwemo VIP, Mpenzi Chocolate, Daktari wa Mapenzi na Nitadumu Naye.

Hata hivyo leo ameshtua watu na maneno aliyoandika kuwa ‘Wakati naanza mziki huu wa kidunia nilikua nina mori balaa kuliko mmasai, ila kila muda ulipokwenda ikawa mori unapungua kisha nikaacha kwa kuwa nilihisi sioni sababu ya kuendelea.

“Cha kushangaza sasahivi nna hamu ya kuimba balaaa, nataka niimbe mpaka nigaregare mwaka huu, nikifika mjini lazima niimbe insha Allah, Mungu akipenda ntaimba ntaimbaaaaa mpaka watu walie kwa furaha. Tatizo nauli tu najichanga nije mjini,’ameandika Mzee Yusufu.

Kutokana na ujumbe huo, Mwanaspoti imemtafuta ili kupata ufafanuzi wa alichokiandika kujua alimaanisha nini haswa.

Katika majibu yake amesema watu waelewe kuwa atarudi tena kabla ya kuanza mwezi mkutukufu wa Ramadhani unatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi wa nne.

Alipoulizwa anarudi kwa staili gani ukizingatia kwamba kwa sasa watu wanajua amejikita kwenye dini, Mzee Yusufu amesema asingependa kuliweka wazi sana isipokuwa kutahusisha uchangishaji wa vyombo vya bendi.

Pia aliongeza ameamua kurudi kwa kuwa ameona kuna fursa nyingi.

Baadhi ya watu walioona ujumbe huo wamekuwa na maoni tofauti akiwemo Waleed Ahmed, amesema siku hizi hadi Qaswida zinakuja na kiki.. New Qaswida loading......

Wakati Kuruthum Seif ameandika’usinambie unataka kurudi kwenye mziki wa kidunia tena, sikuchangii nauli,”

Z.8174 ameandika “Wachana mambo ya kidunia itengeneze Akhera yako, wewe ni Alhaji, wacha kuharibu Hijja yako kaka Yangu, dunia tunapita, imeniuma sana

Immatheboy Masoudy amesema,”Rudi Mzee Yusufu tumekumic sana ulifanya taarabu hata tusiyoipenda tuipende huku bado kuna nafasi yako haijachukuliwa na mtu.