Mzee Yusuph awatega mashabiki

ALHAJI Mzee Yusuph amesema watu waendelee kutabiri wanachotabiri kuhusu kauli yake ya ‘Narudi Mjini’ aliyoandika Machi 12, 2020 katika ukurasa wake wa mtandao Instagram.

Mzee Yusuph ambaye alikuwa mtunzi, mwimbaji na mpiga kinanda katika kundi la muziki wa alilolimiki la kupitia muziki wa taarab la Jahazi alilolimiliki kabla ya kuacha muziki na kuamua kufuata maadili ya dini yake ya Kiislam, ameliambia Mwanaspoti kuwa kitendo cha kutangaza kurudi mjini amepata simu nyingi za watu kutaka ufafanuzi juu ya andiko hilo.

Nyota huyo ambaye sasa amegeuka mtoa mawaidha ya dini sehemu mbalimbali huku pia akiimba kaswida, amesema wapo watu wanaomtajia maeneo wanayoamini ndiyo mazuri kwa ajili ya kufanyia tamasha kubwa la kurejea katika muziki na hata kumpendekezea majina ya wadhamini.

“Yaani sikutegemea mapokezi makubwa ya andiko langu la narudi mjini kupokewa na watu wengi hivi, yaani hadi nimeshangaa, na ningeshangaa zaidi wewe usinipigie simu kuniuliza hili sababu tulikuwa tunakesha wote pindi naimba taarabu hahahaha.. sasa wacha watu waendelee kutabiri jambo hilo wanalodhani la kurudi mjini kwenye taarabu, likifika basi kila mtu atajua,” alisema Alhaji Mzee Yusuf

Alhaji Mzee Yusuf mwaka 2016 alitangaza kuachana na muziki na kuingia kwenye masuala ya kufundisha dini na kutoa dawa kabla ya kwenda kuhiji Makka na jina lake hapo ndipo lilipobadilika na kuanza kuitwa Alhaji.

Awali, Alhaji Mzee Yusuf baada ya kutangaza kuachana na muziki, watu wengi walikuwa wakimuomba arudi kwenye muziki kutokana na muziki wa taarabu kuyumba, lakini alishikilia msimamo wake kuwa muziki huo ni kinyume cha maadili ya dini ya Kiislam.

Lakini sasa, bado giza la ‘Narudi Mjini’ limetanda. Japo ameshindwa kuweka wazi, Alhaji Mzee Yusuf kwenye ukurasa wake wa Instagram, amekuwa akiweka picha za wadau wa muziki wa taarabu na waimbaji baadhi wa muziki huo huku aliandika maneno haya “Narudi mjini” ndugu zangu mnipokee, hapa nawaza nitaimba na wasanii wale wale au nichague wengine, manaa wapo waliokuwa tayari wameshaanzisha bendi zao.

Miungoni mwa waimbaji aliposti picha zao ni Haji Boha aliwahi kuwa kiongozi wa bendi yake ya Jahazi, Prince Amigo, Mtoto pori walikuwa waimbaji wa Jahazi.