Ni mwaka wa watu weusi mashindano ya urembo duniani

Muktasari:

Unaweza kuuita ni mwaka wa watu weusi katika mashindano ya urembo ulimwenguni baada ya mwaka huu mashindano manne makubwa ya urembo kutwaliwa na watu weusi.

Wakati Toni-Ann Singh kutoka nchini Jamaika akitawazwa rasmi kuwa mrembo wa dunia kwa mwaka 2019, ameongeza idadi ya watu weusi kushikilia mataji ya urembo duniani kwa mwaka huu.

Toni-Ann Singh mwenye miaka 23, alitawazwa usiku wa kuamkia leo Jumapili Desemba 15, 2019 nchini Uingereza ambako mashindano hayo yamefanyika.

Kutokana na ushindi huo, anafuata nyayo za watu watatu weusi kushikilia mataji katika mashindano ya urembo duniani kwa mwaka huu.

Mataji mengine yaliyotwaliwa na mtu mweusi ni lile la Miss Universe, shindano lililofanyika Desemba 8, 2019 na mrembo Zozibini Tunzi, kutoka n Afrika Kusini kutwaa taji hilo akipokea kijiti hicho kutoka kwa Catriona Gray kutoka nchini Ufilipino.

Wakati mshindi wa shindano la Miss USA, Cheslie Kryst akiwa mtu mweusi alitwaa taji hilo akilipokea kutoka kwa Sarah Rose Summers.

Kama vile haitoshi, Miss Teen USA, nayo iliwakilishwa vema na Kaliegh Garris huku taji la Miss Amerca likitwaliwa na Nia Franklin.

Mataji haya kwa mwaka 2018 yalikuwa yakishikiliwa na watu weupe kasoro la Miss Teen USA , ambalo Hailey Colborn ndiye alikuwa mtu mweusi pekee alipata ushindi katika mashindano hayo kwa mwaka jana.