Obama, mkewe huwaambia kitu kwa Burna Boy

Muktasari:

Rais mstaafu wa Marekani, Barack Obama na mkewe Michelle wametaja orodha ya wasanii waliowaona wamekuwa bora kwao kwa mwaka 2019 huku jina la msanii kutoka nchini Nigeria, Burna Boy wote wakilitaja japokuwa kwa nyimbo tofauti.

Dar es Salaam. Zikiwa zimepita siku 20 tangu Rais wa 44 nchini Marekani, Barack Obama kutaja orodha ya wasanii anaowaona bora kwa mwaka 2019, mkwewe naye Michelle ametaja wa kwake.

Katika orodha hiyo wawili hao wamejikuta pamoja na kutaja wasanii wengine, msanii Burna Boy amejitokeza kwa wote akiwa msanii kutoka nchi za Afrika.

Wakati katika mtandao wa kijamii wa Twitter Desemba 30, 2019, Obama alitaja nyimbo ya ‘Anything’ kuwa  ndiyo aliouona bora kwake kwa mwaka huo wa 2019 kutoka kwa msanii huyo.

Mkewe Michelle jana Jumapili Januari 19,2020 kupitia ukurasa wake katika mtandao wa kijamii wa Instagram kataja wimbo wa ‘My Money My Baby’ kuwa ndio uliomkosha kutoka kwa msanii huyo anayefanya vizuri kwa sasa Afrika.

Kutajwa kwa msanii huo ambaye jina lake halisi ni  Damini Ebunoluwa Ogulu na kiongozi huyo mkubwa duniani huenda kukazidi kumfungulia milango zaidi katika soko la kimataifa kwani ni kwa mwaka jana pekee na mwaka huu 2020 anashikilia  tuzo zisizopungua nane.

Pia, Nigeria na Afrika kwa ujumla wanamsubiria katika tuzo za Grammy zinazotarajiwa kutolewa mwezi huu ambapo ameingia katika kipengele cha ‘World Best Music Album’ kupitia albamu yake ya nne aliyoipa jina la African Giant yenye nyimbo kali kama ‘On The Low’ na ‘Gbona’.

Tuzo ambazo anashikilia mpaka sasa Burna Boy ni pamoja na ile ya African Muzik Magazine Awards(AFRIMMA) zilizofanyika Oktoba 28,2019, Dallas, Texas nchini Marekani ambapo  alishinda tuzo tatu ikiwemo wimbo bora wa kushirikiana na Wimbo wa mwaka kupitia wimbo wa ‘Killing Dem’ alioimba na msanii Zlatan na msanii bora wa kiume Afrika Magharibi.

Tuzo nyingine ni za Africa Music Awards (AFRIMA) zilizotolewa Novemba 23, 2019 katika ukumbi wa Eko Lagos nchini Nigeria ambapo alishinda kipengele cha msanii bora wa kiume Afrika Magharibi kupitia wimbo wa ‘Ye’ na msanii wa mwaka Afrika kupitia wimbo wake wa Gbona.

Kama vile haitoshi katika tuzo za Soundcity MVP zilizofanyika usiku wa Januari 10,2020 nchini Nigeria, Burnaboy huko nako alishinda tuzo tatu ikiwemo ni msanii bora wa, Msanii bora afrika pamoja na wimbo bora wa mwaka kupitia wimbo wake wa ‘Killin Dem.’

Buna Boy mwenye miaka 28 ambaye ni mwimbaji na mtunzi , jina lake lilipata umaarufu pale alipoachia kibao chake cha kwanza mwaka 2012 alichokipa jina la "Like to Party" katika albamu yake ya kwanza ya L.I.F.E.