Shilole awapa makavu wanaomuwinda mumewe

Muktasari:

  • Shilole avunja ukimya, awatolea uvivu wanawake wanaomuwinda mume wake akisisitiza ametumia nguvu kubwa kumpa mwonekano alionao sasa

Dar es Salaam. Mwanamuziki na mwigizaji wa filamu, Zuwena Mohamed ‘Shilole’ ametumia ukurasa wake wa Instagram kuwapasha wanawake wanaotaka kumchukua mume wake, Uchebe.

Shilole ameeleza namna alivyoanza na mwanamume huyo na jinsi wanawake wa mjini wanavyotaka kuingilia ndoa yake.

Kupitia akaunti hiyo ameandika maneno yanayosomeka,“Niliridhika na hali yako tangu mwanzo mpaka sasa unashaini ila wadangaji msivyo na haya mnaanza kumwambia muwe wangu Uchebe umekuwa handsome (umekuwa mzuri). Mkome namtunza zamani mlikuwa wapi?”

Desemba mwaka 2017, msanii huyo alifunga ndoa na Uchebe - mwanamume ambaye kwa wakati huo hakuwa akifahamika na watu wengi walimkebehi kwa kile kilichodaiwa hana kazi wala shughuli ya kumuingizia kipato, hivyo atalelewa na Shilole.