Tanasha anadai Diamond amemkuza Afrika Mashariki

Muktasari:

  • Kuhusu Diamond kumruhusu kufanya muziki wakati alishajiapiza kuwa hawezi kuwa na mpenzi mwanamuziki, alisema aliona anao uwezo.

Mbali ya kumuona mara moja katika video ya wimbo Nagharamia wa Alikiba, mwanamitindo Tanasha Donna hakuwa maarufu mpaka alipoanzisha uhusiano wa kimapenzi na Diamond Platnumz.

Ni ukweli ambao anaukubali kuwa, Diamond amemtambulisha Tanzania na kumuongezea umaarufu Afrika kwa ujumla.

Akizungumza katika kipindi cha Block 89 kinachorushwa na kituo cha televisheni Wasafi, alisema anamshukuru Diamond kwa kumsaidia kuwa maarufu kwa kuwa imemrahisishia kuingia kwenye muziki na kufanya vizuri.

Tanasha mwenye asili ya Kenya na Ubelgiji, alisema kabla ya kuwa na Diamond, pamoja na kuwa mwanamitindo na mtangazaji, hakuwa maarufu.

“Wimbo wangu Redio umefanya vizuri sana lakini sio kwa nguvu zangu binafsi, umaarufu alionipa na yeye kupush (saidia) katika mitandao yake nimefanya vizuri, huu ni ukweli ambao nitausema siku zote,” alisema.

Akizungumzia tetesi kuwa aliwahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwanamuziki Alikiba kabla ya kukutana na Diamond, alisema siyo kweli na hakuwa kuwa na mawasiliano naye baada ya kazi.

“Wakati tunarekodi mpenzi wangu wa zamani alikuwa hapo anasubiri nimalize kazi na kina Alikiba na Christian Bella. Ni mara ya kwanza na ya mwisho nilikutana na Alikiba pale,” alisema.

Mwanamuziki huyo alisema kwa mara ya kwanza alikutana na Diamond katika club ya usiku jijini Nairobi na mwisho wa siku alimfuata kwa kumuandikia ujumbe katika mtandao wa Instagram.

“Aliponitafuta Instagram nilishtuka kwa sababu Diamond ni staa, nikajiuliza ni wangapi anawafuata kwa staili hiyo lakini baadaye nikagundua kuwa ni mtu mzuri mwenye nia njema na mimi,” alisema.

Kuhusu Diamond kumruhusu kufanya muziki wakati alishajiapiza kuwa hawezi kuwa na mpenzi mwanamuziki, alisema aliona anao uwezo.

“Nilimsikilizisha nyimbo zangu pia aligundua kuwa nina kipaji akasema mimi ni nani mpaka nikuzuie kutimiza ndoto zako,” alisema.

Kuhusu ndoa amesema kwa sasa hawajafirikia kwa kuwa wameamua kwanza kuimarisha penzi lao.

“Mimi ni Mkristo na Diamond ni Muislam, tumekubaliana kwamba kila mtu atabaki na imani yake, ingawa kwa sasa suala la ndoa tumeliweka pembeni kwanza,” alisema.