Wema: Walionibeza wananiomba dawa nao wapungue

Muktasari:

Wema ni mshindi wa taji la Miss Tanzania 2006 pia ni mmoja waingiza wakubwa katika tasnia ya filamu

Dar es Salaam.Mwanamitindo na mcheza filamu, Wema Sepetu amesema waliokuwa wanamkejeli kuhusu kupungua kwa mwili wake sasa wanaomba dawa anayotumia ili nao wawe na mwili kama wake.

Wema amesema kuna wakati alikuwa anakosa amani kutokana na maneno ya watu wakiwamo wasanii wenzake waliokuwa wakimrushia vijembe kwa kubadili mwili wake, lakini sasa wanamsumbua kutaka dawa kwake.

"Miezi kadhaa nyuma nilipokuwa na mwili mnene watu walikuwa wakinibeza sana, hata wasanii wenzangu, lakini sasa hivi kutokana na kukondeana huku, wameukubali wembamba wangu na kunisumbua kutaka dawa niliyotumia kwani nimependeza," alisema Wema.

Wema alisema hata watu wa mtandao wa Instagram waliokuwa wakimshambulia mwili wake kwa kutaka kuurudisha mwili wa zamani (unene), nao wanamuomba awatajie alichotumia kwani amependeza.