Upandikizaji ogani ya figo

Katika sehemu ya matibabu, mashine ya dialysis ni kifaa tiba mbadala cha figo zilizoshindwa kufanya kazi au kuharibika.

Leo nitazungumzia upandikizaji wa figo kama sehemu ya tiba ya ugonjwa sugu wa figo.

Ogani za mwilini ikiwamo figo, moyo, mapafu na ini pale zinapoharibika na kushindwa kufanya kazi yake moja ya njia ya kimatibabu kwa mgonjwa ni upandikizaji wa ogani hiyo.

Kwa wagonjwa wa figo wenye tatizo sugu au kuharibika na kushindwa kufanya kazi matibabu yenye matokeo mazuri ni upandikizaji wa figo.

Kwa wagonjwa wote ambao wanavigezo vinavyotakiwa wanaweza kufanyiwa upasujaji na kuwekewa figo mpya.

Lakini ni jambo la kawaida kuona matumizi ya mashine ya dialysis yanatumika zaidi, hii ni kutokana na upandikizaji una changamoto ikiwamo upatikanaji wa figo toka kwa wanaojitolea.

Vile vile madaktari wanaofanya upasuaji huu ni wachache na pia vifaa tiba huwa ni changamoto katika nchi zenye uchumi mdogo mpaka wa kati.

Ukilinganisha na mashine ya dialysis upandikizaji wa figo unaleta nafuu haraka zaidi na kuboresha maisha ya mgonjwa na kuyarefusha zaidi. Figo hizi hupatikana kwa watu waliofariki ikiwamo katika ajali walioacha ujumbe na kukubali kwa hiari yao viungo vyao vitumike kusaidia wengine.

Pia, wapo watu ambao wanaweza kujitolea figo zao na kuamua kubaki na moja na kuwapa wagonjwa wa figo.

Gharama za upandikizaji ni kubwa duniani kote. inakadiriwa kuwa ni kati ya Dola 25,000 hadi 50,000 za Marekani kwa nchi za Afrika Kusini na India ambazo mara nyingi wagonjwa wanaotoka Tanzania wanakwenda huko kutokana na unafuu wa gharama ikilinganishwa na nchi za Ulaya.

Kwa kawaida ni figo moja mpya huhitajika kuwa mbadala wa figo mbili zilizoharibika kabisa na kushindwa kufanya kazi ya kuondoa taka sumu katika damu.

Ni lazima figo mpya anayowekewa mgonjwa iendane na figo zake vinginevyo itamlazimu kusubiri mpaka ipatikane figo inayoendana nayo.

Mwandishi wa makala haya ni daktari wa binadamu