“Sina khanga, dela wala mipira, lakini naomba kura”

Mgombea Ubunge jimbo la Ukonga (Chadema) Asia Msangi

Muktasari:

  • Asia Msangi anagombea ubunge jimbo la Ukonga kupitia Chadema wakati CCM, wao wamempitisha Mwita Waitara kuwania nafasi hiyo.

Dar es Salaam. Mgombea Ubunge jimbo la Ukonga (Chadema) Asia Msangi amesema anaomba kura lakini hana khanga, dela, mipira wala jezi.

Akizungumza leo Septemba 12 katika kampeni za lala salama za jimbo hilo, Msangi amewataka wananchi kumchagua kwa ridhaa yao.

“Nikikuletea elfu mbili ili unichague nitakuwa nimekudharau sana hivyo naomba nikuheshimu unichague kwa ridhaa yako mwenyewe,” amesema na kuongeza:

“Mimi ni mwanamke ninayejiamini, sio mwoga, sitishwi na kikubwa zaidi sina bei.”

Msangi amesema atakwenda bungeni kupambana na kwa kuwa atakwenda bila kutoa fedha, atafanya kazi kama punda.

“Tambueni kwamba mmepata mwakilishi makini anayejiamini na ambaye hana njaa. Ukonga ina changamoto nyingi, nipeni ridhaa nikazishughulikie nikajengee hoja,” amesema.

Amesema atahakikisha anasimamia fedha za mfuko wa jimbo  ili kuchochea maendeleo ya Ukonga .

“Niwaambie kwamba Asia Msangi huwezi kumteka kirahisi yaani utoke Tarime uje uniteke mimi sasa nawaambia huyo aliopewa ramani ya kuniteka namkaribisha nyumbani kwangu Kitunda Relini na ninakuwepo kuanzia saa nne usiku aje,” amesema.