CCM yawateua Kalanga, Waitara kugombea ubunge

Muktasari:

  • Watagombea kwenye majimbo walikojiuzulu ubunge kwa tiketi ya Chadema

Dar es Salaam. Kamati Kuu maalumu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM imewateua Julius Kalanga na Mwita Waitara kuwa wagombea ubunge katika majimbo walikojiuzulu.

Katika kikao kilichofanyika leo Agosti 14, 2018 ofisi ndogo za chama hicho jijini Dar es Salaam, Kalanga ameteuliwa kugombea ubunge Monduli ambako alikuwa mbunge kwa tiketi ya Chadema kabla ya kujiuzulu na kuhamia CCM.

Waitara amerejeshwa kuwa mgombea jimbo la Ukonga alikokuwa mbunge kwa tiketi ya Chadema.

Kamati kuu ya CCM pia imemteua Timotheo Mzava kuwania ubunge Korogwe Vijijini, ambako aliyekuwa mbunge Stephen Ngonyani maarufu Majimarefu alifariki dunia.

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) imeshatangaza uchaguzi katika majimbo hayo utafanyika Septemba 16, 2018.

Kamati Kuu kupitia kwa Mwenyekiti wa CCM, Rais John Magufuli imewashukuru wananchi waliojitokeza kushiriki katika uchaguzi mdogo wa jimbo Ia Buyungu na kata 77 na kukipa dhamana chama hicho na wagombea wake na kuwawezesha kushinda kwa asilimia 100.

CCM katika taarifa iliyotolewa na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Humphrey Polepole imesema kushinda katika uchaguzi ni jambo moja, kuwatumikia wananchi kwa unyenyekevu, uaminifu na kujitoa kushughulika na shida za watu ni jambo jingine.