Chadema washtushwa taarifa za Millya kujiuzulu

James Millya.

Muktasari:

  • Barua ya kujizulu ubunge ya James Millya inayosambaa mitandaoni imekishtua chama chake cha Chadema kikishindwa kueleza kama ni kweli amehamia CCM au la.

Arusha. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeeleza kushtushwa na taarifa za mbunge wake wa Simanjiro mkoani Manyara, James Millya kujiuzulu.

Katibu wa Chadema Kanda ya Kaskazini, Aman Golugwa akizungumza na Mwananchi leo Oktoba 7, 2018 amesema hana taarifa za kujiuzulu kwa Millya.

"Nimeulizwa na mtu mwingine muda si mrefu juu ya hizi taarifa, mimi sina kwa uhakika ila ngoja nimtafute Millya," amesema.

Amesema chama hicho kitatoa taarifa rasmi mara baada ya kujiridhisha na uamuzi huo wa Millya.

Hata hivyo, Millya mwenyewe hakupatikana kuelezea barua inayosambaa kuwa amejiuzulu kutokana na kuzima simu zake.

Hata hivyo, mapema wiki hii akizungumza na Mwananchi, Millya alieleza kutoridhishwa na baadhi ya mambo ndani ya Chadema.

Alisema ndani ya Chadema hali si nzuri kwani si rahisi tena kukosoana juu ya mambo mbalimbali bila kueleza kwa kina mambo hayo.