Kimenuka Kenya, Kenyata awafokea washirika wa Rutto hadharani

Muktasari:

Jumapili iliyopita Rais Kenyatta alitumia lugha ya Kikuyu kuwatuhumu viongozi wa chama cha Jubilee na kusema kwamba hatishiki

Nairobi, Kenya. Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta ameapa kuanza kampeni ya kuzima wanasiasa wa kundi linalo hujumu uongozi wake maarufu kama (Tangatanga).

Rais Kenyatta aliyekuwa akizungumza na waumini wa dhehebu la Akorino katika Uwanja Kasarani Jumapili iliyopita alionekana mwenye hasira na kutumia lugha ya Kikuyu.

Rais Kenyatta alionekana kuwalenga wanasiasa ambao wanamuunga mkono Naibu wa Rais, William Ruto kuwania urais mwaka 2022.

“Leo ninazungumza kwa lugha ya nyumbani, nitaenda katika eneo langu (la Mlima Kenya) kuwaambia watu kile ambacho wanafanya.

“Wanafaa kujua kwamba si wao walionifanya kuwa Rais, bali mimi ndiye niliyewafanya kupata viti. Wakenya ndio walionichagua na nitaendelea kusimama na ukweli hadi nikamilishe kazi mliyonipa.

“Wanafikiri kwamba nikiwa kimya, wamefaulu kuninyamazisha, nimesema kwamba sitaki siasa na hiyo ndiyo maana sijawatimua katika maeneo waendayo,” alisema.

Alisema baadhi ya wanasiasa hasa wa chama cha Jubilee, wamekaidi wito wake wa kutaka wasitishe kampeni za mapema na badala yake watumikie Wakenya.

Kenyatta alisema viongozi hao ‘wakora’ wamekataa kuunga mkono juhudi zake za kutaka kuunganisha nchi kupitia kukutana kwao na Raila Odinga walipopena mikono maarufu (handisheki).

“No riu ningwaria na Gikuyu, aya nimeke uria mekaga maturaga manumaga ni uhoro wao gutiri kundu maratutwara (Leo ninazungumza kwa lugha ya Kikuyu, acha viongozi hao wafanye wanachofanya lakini sitishiki,” alisema Rais Kenyatta.

Alisema hana haja ya kung’ang’ania madaraka lakini lengo lake kuu ni kumaliza siasa za ukabila ambazo alisema zimegawanya nchi kwa muda mrefu.

“Sina mpango wa kuiba fedha za umma lakini nitahakikisha kuwa ninaacha nchi iliyoungana na kila Mkenya anaweza kwenda popote bila uwoga,” alisisitiza Kenyatta.

Alisema atazunguka kote nchini kuwamaliza kisiasa wanaopinga hatua hiyo ya kupeana mkono na Raila kwa kuhimiza Wakenya wasiwachague katika uchaguzi ujao.

Aidha, Kenyatta aliwataka viongozi hao ambao wameanza siasa za 2022 kuacha mara moja na kuwatumikia wananchi.