Mwanamke mwenye umri wa miaka 80 abakwa na kuuawa

Muktasari:

  • Mwanamke wa miaka 80 amekutwa amebakwa na kuuawa katika kijiji cha Kanyange, Kata ya Kirinyaga.

Jedidah Wanjiru Jumatatu asubuhi alikutwa amelala sakafuni ndani ya nyumba yake na mdomo wake umejaa nguo.

Alikuwa na michubuko shingoni, ikionyesha kwamba alikabwa hadi kufa. Mlango haukuvunjwa na wanafamilia walishuku kuwa wauaji waliweza kuingia ndani ya nyumba Jumapili usiku kabla ya marehemu ambaye alikuwa akiishi peke yake kwenda kulala.

Mtoto wa marehemu, Stephen Weru, alisema, alikwenda kukamua maziwa ya ng'ombe kwa ajili ya mama yake na akakuta mlango umefunguliwa akashuku kuwa kuna kitu kibaya kimetokea."Wakati naingia nilimuona mama yangu chumbani akiwa amekufa, nilishtuka mno," alisema Bw Weru.

Haraka aliwaambia wanafamilia wengine na tukio hilo limeripotiwa kwa Kituo cha Polisi cha Baricho. Muda kidogo baadaye, polisi walifika eneo la tukio na kuchukua mwili wa mwanamke huyo na kupeleka kwenye chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ya Jamii.

Ndugu wa mwanamke huyo, Bwana Muriuki Kamakia, alisema hakuna chochote kilichoibiwa kutoka kwa marehemu. "Nadhani wauaji walikuwa na nia ya kumuua dada yangu tu kwa sababu vitu vyote vya nyumbani vilikuwa sawa,hakuna kilichoibiwa," akasema Bw Kamakia.

Familia hiyo sasa inahitaji haki kufuatia mauaji ya kikatili ya ndugu zao. "Tunataka suala hilo lichunguzwe na wauaji wafikishwe katika vyombo vya dola," alisema Bw Joseph Wachira, mtoto wa kwanza wa marehemu.

Msaidizi wa Mkuu wa polisi Bw Moses Muriuki alisema alikuwa nyumbani wakati alipopokea ripoti kwamba mzee huyo ameuawa."Wakati niliposikia kilichotokea, nikakimbilia katika eneo la tukio na kukuta ntu huyo amekufa ndani ya nyumba yake.

Aliwataka wakazi kushirikiana na polisi na kutoa taarifa zozote ambazo zinaweza kusababisha kukamatwa kwa wauaji hao.