Papa ataka makasisi mashoga kuondoka kanisani

Muktasari:

  • Hilo pia linahusu wanawake wanaotaka kuingia katika jamii za wanawake wa kidini ambao wanataka kuwa watawa. Katika kanisa Katoliki, makuhani, makasisi na watawa kutakiwa kula kiapo cha kutooa wala kuolewa.

Vatican City, Vatican. Mkuu wa Kanisa la Katoliki Duniani, Papa Francis amesema wanaume wenye hulka ya ushoga wasiruhusiwe kuwa makasisi wa kanisa hilo na amewataka wenye tabia hiyo kujiondoa badala ya kuishi maisha ya undumilakuwili.
Japokuwa aliwahi kuzungumzia juu ya haja ya kuwachunguza na kuwachuja watu wa kuishi maisha ya kidini, maoni yake haya yaliyomo kwenye kitabu kipya yanayosisitiza makasisi ambao hawawezi kuishi kwa kuzingatia viapo vyao vya useja waondoke yametoa ufafanuzi unaoeleweka kwa sasa.
Papa Francis ametoa maoni hayo katika mahojiano marefu ya kitabu hicho aliyofanya na kasisi wa Hispania Fernando Prado yaitwayo 'Nguvu ya wito' ambamo anazungumzia kwa kirefu changamoto za kuwa kasisi au mtawa.
Papa Francis amesema katika kitabu hicho kwamba ushoga kanisani ni jambo analohofia.
Kitabu hicho kinatarajiwa kuchapishwa wiki hii katika lugha kadhaa. Shirika la Reuters limepata nakala ya awali iliyochapishwa kwa kitaliano.
"Suala la ushoga ni jambo baya sana," amesema na akaongeza kwamba wale walioaminiwa kuwachuja wanaume kuwa makasisi lazima wawe na uhakika kwamba waliopitishwa ni wanadamu na waliokomaa kihisia kabla ya kuwekwa wakfu.
Hilo pia linahusu wanawake wanaotaka kuingia katika jamii za wanawake wa kidini ambao wanataka kuwa watawa. Katika kanisa Katoliki, makuhani, makasisi na watawa wanakula kiapo cha kutooa wala kuolewa.