Rais wa Sudan alipiga chini Baraza la Mawaziri

Muktasari:

  • Ni kutokana na mzozo wa kiuchumi baada ya mfumuko wa bei kufikia asilimia 65

Khartoum, Sudan. Rais wa Sudan, Omar la Bashir amevunja Baraza la Mawaziri na akamteua Waziri Mkuu mpya ikiwa ni hatua ya kukabiliana na mzozo wa kiuchumi baada ya mfumuko wa bei kufikia asilimia 65.
Uamuzi wa kuvunja baraza hilo lililokuwa na mawaziri 31 akiwamo Waziri Mkuu Bakri Hassan Saleh uliridhiwa na chama tawala cha National Congress Party (NCP).
"Hali ya uchumi inahitaji kupatiwa ufumbuzi na kutokana na hilo Rais Bashir ameamua kupunguza ukubwa wa serikali yake katika ngazi zote," msaidizi wa Bashir aliwaambia waandishi wa habari.
"Badala yake Rais Bashir ameamua kuwa na baraza dogo lenye mawaziri 21,” aliongeza.
Baada ya kuvunja Baraza la Mawaziri lililokuwa linaongozwa na Saleh, Rais Bashir alimteua Motazz Moussa kuwa Waziri Mkuu mpya ambaye anachukua nafasi ya Saleh aliyechaguliwa mwaka 2017.
Kabla ya kuteuliwa nafasi hiyo, Moussa alikuwa waziri anayeshughulikia masuala ya umeme na umwagiliaji.
Ingawa nchi hiyo iliyogubikwa na migogoro ilirekodi ukiuji wa uchumi kwa asilimia sita kati yam waka 1998 na 2008, ilipoteza hazina yake ya mafuta baada ya Sudan Kusini kujipatia uhuru mwaka 2011.
Hakuna nafasi nyingine za mawaziri zilizotangazwa, lakini idadi ya mawaziri katika serikali mpya itapungua mpaka 21 kutoka 31, hatua ambayo inalenga kupunguza matumizi.
Awali Naibu Mwenyekiti wa chama cha NCP aliwaambia waandishi wa habari kwamba Mawaziri wa Mambo ya Nje, Ulinzi na masuala ya Rais watabaki katika nafasi zao, pindi litakapoundwa baraza jipya la mawaziri.