Rubani afa baada ya helikopta kuanguka juu ghorofa Marekani

Muktasari:

  • Helkopta hiyo ya injini mbili ilianguka dakika 11 bada ya kuanza safari ilikuwa ikitokea Manhattan kuelekea uwanja wa ndege wa Linden mjini New Jersey

Manhattan, Marekani. Rubani, Tim McCormack amefariki dunia baada helikopta aliyokuwa akiendesha kupata itilafu na kuanguka juu ya jumba la ghorofa 54 mjini Manhattan.

Ajali hiyo ilitokea jana mchana katika barabara ya 787, kaskazini mwa ukumbi wa Times Square ambako helikopta hiyo ililipuka na kushika moto mara baada ya kugonga kituo cha AXA Equitable.

Watu walioshuhudia ajali hiyo wanasema jumba hilo lilitetemeka wakati ndege hiyo ilipoanguka juu yake na kusababisha hofu kwa wananchi walioofananisha tukio hilo na mashambulizi ya kigaidi ya Septemba, 2001.

Kwa mujibu wa taarifa ya maafisa wa kitaifa wa usalama wa anga Marekeni, wanafuatialia ajali hiyo ili kufahamu kama inatokana na matukio ya kigaidi.

“Ajali hiyo siyo ya kawaida, helikopta ilihitaji kibali maalum kutoka uwanja wa LaGuardia mjini New York City jambo ambalo halikufanywa na rubani huyo,” alisisitiza afisa wa usalama wa anga, De Blasio.

Afisa huyo alisema ndege hiyo ya injini mbili chapa Agusta A109E, ilikuwa na rubani pekee ikitokea Manhattan kuelekea uwanja wa ndege wa Linden mjini New Jersey, hata hivyo, dakika 11 baada ya kuanza safari ilianguka juu ya jumba hilo.

Meya wa jiji la New York City Bill de Blasio alisema kuwa helikopta hiyo imeharibiwa kabisa kutokana na jinsi ilivyogonga chini kwa nguvu.

Jengo hilo liko nusu maili kutoka Jumba la Trump Tower, na usafiri wa anga katika maeneo hayo umedhibitiwa kwasababu jengo hilo linamilikiwa na Donald Trump ambeye sasa ni rais wa Marekani.